Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akipokea Tuzo ya kuwa Kinara wa
Dhana ya Urekebishaji wa Wafungwa Magerezani kutoka kwa Waziri wa Mambo ya
Ndani ya Nchi Mhe. Patrobas Paschal Katambi pamoja na Kamishna Jenerali wa
Magereza Jeremia Yoram Katungu kwenye hafla ya hafla ya kuhitimisha Mafunzo ya
Uongozi Ngazi ya Juu Kozi namba 28 na Uongozi Daraja la Pili Kozi namba 48 ya
mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga
Jijini Dar es Salaam Mei 9, 2026.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akionesha tuzo hiyo...........................................
KWA mara ya
kwanza tangu kuanzishwa kwa Jeshi la Magereza Tanzania, mkuu wa nchi, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan ametunukiwa Tuzo Maalumu
ya Kinara wa Dhana ya Urekebishaji wa Wafungwa Magerezani (Champion of Prisoner
Rehabilitation Concept Award) hatua inayotajwa kuwa ishara ya mageuzi makubwa
ya kifalsafa, kiutendaji na kimaendeleo ndani ya mfumo wa haki jinai nchini.
Tuzo hiyo
aliyokabidhiwa Rais Samia, Mei 9, 2026 katika Chuo cha Taaluma ya
Urekebishaji Tanzania haionekani tu kama pongezi kwa uongozi wa Serikali, bali
kama alama ya mabadiliko ya kihistoria yanayoibadilisha falsafa ya magereza kutoka
mfumo wa adhabu kwenda mfumo wa urekebishaji, elimu na maendeleo ya binadamu.
Mageuzi hayo
yanasimamiwa kwa karibu na Mkuu wa Jeshi la Magereza nchini, CGP Jeremiah Yoram
Katungu, ambaye chini ya uongozi wake jeshi hilo limeendelea kufanya maboresho makubwa
ya kiutendaji, matumizi ya teknolojia na utoaji wa mafunzo ya kisasa ya
urekebishaji.
Kwa mujibu
wa wachambuzi wa maendeleo, hatua hiyo inaonesha Tanzania inaanza kuachana na
mfumo wa kikoloni ulioliona gereza kama sehemu ya mateso na kuingia katika mfumo
mpya unaomtazama mfungwa kama binadamu mwenye uwezo wa kubadilika na kuchangia
maendeleo ya taifa.
KUTOKA MFUMO
WA ADHABU KWENDA MFUMO WA UTU
Katika kipindi cha ukoloni, mfumo wa Tanganyika Prisons Service ulijikita zaidi katika kazi ngumu na matumizi ya wafungwa kama nguvu kazi ya bei nafuu kwenye mashamba ya serikali, ujenzi wa barabara, useremala na shughuli nyingine za mikono.
Lakini baada
ya uhuru, hasa kuanzia mwaka 1974, Tanzania ilianza rasmi mageuzi ya kifalsafa
yaliyolenga kubadili mfumo wa magereza kutoka adhabu kwenda urekebishaji tabia.
Mageuzi hayo
yalienda sambamba na kutenganishwa kwa Magereza na Jeshi la Polisi pamoja na
kuanzishwa kwa taasisi maalumu za taaluma ya urekebishaji.
Hapo ndipo
falsafa ya Humanism au utu wa binadamu ilipoanza kuonekana ndani ya mfumo wa
haki jinai nchini.
Katika
falsafa hiyo, hata mfungwa ana haki ya kupewa elimu, kuheshimiwa na kuandaliwa
kurejea katika jamii akiwa mtu bora zaidi.
Ndiyo maana
kwa sasa Jeshi la Magereza limejikita katikamafunzo ya
ufundi, elimu ya tabia, kilimo, uzalishaji na stadi mbalimbali za maisha.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri
Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikagua Gwaride mara baada ya
kuwasili katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga.
......................................
CHUO CHA
UREKEBISHAJI NA UJENZI WA RASILIMALI WATU
Miongoni mwa
taasisi zilizopewa jukumu kubwa la kusimamia mageuzi hayo ni Chuo cha Taaluma
ya Urekebishaji Tanzania ambacho kimeendelea kutoa mafunzo ya Sayansi ya Urekebishaji
kuanzia ngazi ya Astashahada hadi Stashahada.
Kupitia chuo
hicho, maafisa wa Magereza wanafundishwa taaluma za kisasa zinazolenga kubadili
tabia za wahalifu na kuwaandaa kurejea katika jamii kama raia wema.
Wataalamu wa
maendeleo kama vile Theodore Schultz na Gary Becker wanaeleza kuwa maendeleo ya
taifa hayawezi kupatikana bila kuwekeza katika elimu, maarifa na stadi za watu.
Kupitia
Nadharia ya Maendeleo ya Rasilimali Watu (Human Capital Theory), wasomi hao
waliamini kuwabinadamu ndiye mtaji mkubwa wa taifa, hivyo hata watu waliowahi
kufanya makosa wanaweza kubadilishwa na kuwa nguvu kazi yenye mchango katika
uchumi ikiwa watapatiwa elimu, mafunzo na mazingira ya kujitegemea.
Kwa mtazamo
huo, gereza linaanza kubadilika kutoka eneo la kufungia watu kwenda kituo cha
kuandaa nguvu kazi yenye maarifa, nidhamu na uwezo wa kujitegemea baada ya
vifungo.
Mfumo huo
tayari umetumiwa kwa mafanikio katika baadhi ya nchi zilizoendelea. Mfano,
nchini Norway, Gereza la Halden hutumia falsafa ya urekebishaji badala ya
adhabu kali.
Wafungwa
nchini Norway hupewa elimu, mafunzo ya kazi, ushauri wa kisaikolojia na
mazingira yanayofanana na maisha ya kawaida ya jamii.
Kutokana na
mfumo huo, Norway imekuwa miongoni mwa nchi zenye kiwango kidogo zaidi cha
wafungwa kurudia uhalifu baada ya kutoka gerezani.
Sweden mfumo
wa magereza umejengwa katika falsafa ya kurejesha utu wa binadamu na kuwaandaa
wafungwa kurudi kwenye jamii wakiwa raia wema.
Kupitia
elimu ya ufundi, ushauri nasaha na programu za kazi, taifa hilo limefanikiwa kupunguza
msongamano wa wafungwa na viwango vya uhalifu wa kujirudia.
Ni wazi kuwa
mageuzi yanayoendelea ndani ya Jeshi la Magereza Tanzania yanaanza kufuata
mkondo huo wa kimataifa wa kuyafanya magereza kuwa vituo vya ujenzi wa
rasilimali watu badala ya maeneo ya adhabu pekee.
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiangalia kiatu
ambacho kimetengenezwa na Kiwanda cha viatu cha Gereza la Karanga, Moshi mkoani
Kilimanjaro wakati alipotembelea mabanda ya maonesho katika Chuo cha Taaluma ya
Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga Jijini Dar es Salaam.
.......................................
MAOFISA WA
MAGEREZA WABEBA DIRA YA MAGEUZI
Mbali na
sera za Serikali, mafanikio hayo yanaelezwa kuchangiwa pia na maofisa wa Jeshi
la Magereza wanaotekeleza kwa vitendo maono ya mageuzi hayo.
Akifungua
mafunzo ya matumizi ya mfumo wa GAMIS Mei 19, 2026, Kamishna wa Sheria na
Uendeshaji wa Magereza, CP Nicodemus Tenga, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la
Magereza Tanzania, alisema matumizi ya TEHAMA ni sehemu ya maboresho
yanayolenga kuongeza uwajibikaji na ufanisi katika usimamizi wa mali za
Serikali.
“Ni
matarajio ya Jeshi baada ya mafunzo haya wataalamu wa ununuzi watakuwa na
maarifa mapya ya kutumia mfumo wa GAMIS na kuongeza uwajibikaji pamoja na kuboresha
utunzaji wa kumbukumbu,” alisema CP Tenga.
Kauli hiyo
inaonyesha namna Jeshi la Magereza linavyoingia katika falsafa ya Modern State
Theory inayosisitiza matumizi ya teknolojia, uwazi na taasisi imara katika
kuleta maendeleo ya kisasa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi Jeshi la Magereza, ACP Henry Masawe, alisema mafunzo hayo yanalenga kuwawezesha wagavi kusimamia kwa ufanisi mali zote za kudumu za Serikali kupitia mifumo ya kidigitali.
Kauli za
viongozi hao zinaonyesha kuwa mageuzi ya Magereza hayapo tu kwenye maneno ya
kisera, bali yanatekelezwa kwa vitendo kupitia mafunzo, usimamizi wa kisasa na
ujenzi wa uwezo wa watendaji wake.
MAGEUZI
KUTOKA ADHABU HADI UREKEBISHAJI
Wataalamu wa
sera za maendeleo wanaamini kuwa mfumo mpya wa Magereza Tanzania unaendana na
falsafa ya Rehabilitation versus Punishment ambayo imeanza kupewa nafasi kubwa
duniani.
Katika mfumo
huo, gereza halionekani tena kama sehemu ya kuumiza au kulipiza kisasi, bali
mahali pa kubadili tabia na kuandaa maisha mapya.
Ndiyo maana
chini ya uongozi wa Rais Samia, Serikali imeagiza kuanzishwa kwa mfuko maalumu
wa mitaji kwa wafungwa wanaomaliza vifungo vyao wakiwa na ujuzi wa ufundi.
Hatua hiyo
imepokelewa kama utekelezaji wa Nadharia ya Uwezeshaji Jamii (Empowerment Theory)
inayosisitiza kuwa maendeleo ya kweli yanahitaji kuwawezesha watu kujitegemea kiuchumi.
WADAU WAUNGA
MKONO MAGEUZI
Wakili
Hassan Kiangio amesema mfumo huo mpya unaonyesha kuwa mtu aliyepo gerezani
hayupo kwa ajili ya kuadhibiwa pekee, bali kurekebishwa ili aweze kurejea
katika jamii akiwa na maadili na stadi za maisha.
Naye Wakili
Msomi Aloyce Komba amesema mageuzi hayo yanaendeleza juhudi za muda mrefu za
kuboresha haki za wafungwa na mazingira ya magereza nchini.
Kwa upande
wake, Kamanda wa Polisi Mstaafu Jamal Rwambow amesema matumizi ya nishati safi,
utoaji wa vyeti vya ufundi na kujitegemea kwa magereza ni ushahidi kuwa jeshi hilo
linaendana na maono ya maendeleo endelevu.
Mdau wa
maendeleo Majaliwa Mbassa amesema wafungwa wanapopata elimu na stadi mbalimbali
wanageuka kuwa nguvu kazi yenye tija kwa taifa badala ya kuwa mzigo kwa jamii.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri
Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na Wahitimu wa
Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu Kozi namba 28 na Uongozi Daraja la Pili Kozi
namba 48 ya mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania
(TCT) Ukonga Jijini Dar es Salaam.
.......................................
TASWIRA MPYA YA MAGEREZA TANZANIA
Kwa ujumla,
mageuzi yanayoendelea ndani ya Jeshi la Magereza yanaonyesha Tanzania inaanza
kujenga mfumo mpya wa haki jinai unaounganisha utu wa binadamu, elimu, teknolojia,
uzalishaji na maendeleo ya kijamii.
Katika mfumo
huo mpya, maofisa wa Magereza hawabaki tena kuwa walinzi wa wafungwa pekee,
bali wanageuka kuwa walimu, washauri na wajenzi wa mabadiliko ya kijamii. Hii
ni tofauti kubwa na mfumo wa zamani wa magereza uliorithiwa kutoka ukoloni
ambapo askari alionekana zaidi kama msimamizi wa adhabu na nidhamu.
Katika
falsafa ya kisasa ya urekebishaji, askari wa Magereza anatakiwa kumsaidia
mfungwa kubadili mtazamo wa maisha, kupata maarifa mapya na kujiandaa kurejea
katika jamii akiwa mtu mwenye mchango chanya.
Kwa mfano,
Japan, mfumo wa magereza umejengwa katika misingi ya nidhamu, elimu na malezi
ya tabia.
Maofisa wa Magereza
hushiriki moja kwa moja katika kufundisha maadili ya kazi, usafi, muda na
uwajibikaji. Wafungwa wengi hupewa ratiba maalumu za kazi, elimu na mafunzo ya
ufundi chini ya usimamizi wa karibu wa maofisa wa Magereza wenyewe.
Mfumo huo
umeisaidia Japan kuwa na kiwango cha chini cha uhalifu wa kujirudia ukilinganisha
na mataifa mengi duniani.
Mfano
mwingine ni nchini Canada ambapo mfumo wa Correctional Service Canada unawataka
maofisa wa Magereza kuwa sehemu ya mchakato wa marekebisho ya wafungwa.
Askari
hupatiwa mafunzo ya saikolojia ya tabia, ushauri nasaha na namna ya
kushughulika na watu wenye changamoto tofauti za kijamii. Ndani ya mfumo huo,
askari si mtu wa kutoa amri pekee, bali anakuwa mshauri anayemsaidia mfungwa
kujenga mpango wa maisha ya baada ya kifungo.
Katika
baadhi ya magereza ya Canada, maofisa hushiriki pamoja na wafungwa kwenye
programu za elimu, mafunzo ya kazi na hata mijadala ya kijamii inayolenga
kujenga uwajibikaji na kuondoa tabia ya vurugu.
Nchini
Singapore, mfumo wa magereza umejengwa katika falsafa inayojulikana kama
“Captains of Lives”. Kupitia mfumo huo, maofisa wa Magereza wanafundishwa kuona
kazi yao si kufunga watu pekee, bali kusaidia kubadili maisha yao.
Serikali ya
Singapore inaamini askari wa Magereza ni viongozi wa mabadiliko ya kijamii
wanaoweza kusaidia kupunguza uhalifu kwa kuwajenga wafungwa kitabia na
kitaaluma.
Kutokana na
mfumo huo, wafungwa wengi nchini humo hupata mafunzo ya teknolojia, biashara
ndogo, ufundi na elimu ya kawaida kabla ya kutoka gerezani.
Mfano
mwingine unaotajwa sana ni nchini Netherlands ambako baadhi ya magereza
yamepunguza matumizi ya mfumo mkali wa kufungia wafungwa muda wote na badala
yake kuwekeza katika elimu, ushauri wa kisaikolojia na maandalizi ya maisha ya
baada ya kifungo.
Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Jacob Mkunda na Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Camillius Wambura wakiwa kwenye hafla hiyo.
.....................................................
Maofisa wa Magereza katika mfumo hufanya kazi karibu sana na wafungwa kama walezi na wasimamizi wa maendeleo yao binafsi.
Kutokana na
mafanikio ya mfumo huo, baadhi ya Magereza nchini humo yamefungwa kutokana na
kupungua kwa idadi ya wafungwa na viwango vya kurudia uhalifu.
Hata
Tanzania sasa inaanza kuelekea katika mfumo huo wa kimataifa.
Kupitia Chuo
cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania, maofisa wa Magereza wanafundishwa sayansi
ya urekebishaji, usimamizi wa wafungwa kwa kuzingatia utu wa binadamu na mbinu
za kisasa za marekebisho ya kijamii.
Hivyo, Askari wa Magereza wa sasa anaanza kuwa zaidi ya mlinzi wa gereza. Anakuwa:
mwalimu wa
stadi za maisha, mshauri wa kitabia,
mlezi wa
matumaini ya mfungwa, na daraja la kumrudisha mfungwa katika jamii akiwa raia mwema
na mwenye uwezo wa kujitegemea.
Kwa mtazamo
wa maendeleo, huu ndiyo mfumo ambao mataifa mengi yaliyoendelea yameanza
kuutumia kwa sababu unaamini kuwa usalama wa jamii haupatikani kwa adhabu kali
pekee, bali kwa kujenga binadamu mwenye maadili, elimu na matumaini ya maisha
mapya.
Na huenda
hiyo ndiyo sababu kubwa iliyofanya Jeshi la Magereza
Tanzania kuona umuhimu wa kutoa tuzo hiyo kwa mara ya kwanza katika historia
yake — kama ishara ya kuthamini mageuzi yanayobadili si tu magereza, bali pia
falsafa nzima ya maendeleo ya binadamu Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi mbalimbali mara baada ya kuwasili katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga.
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na
Mfungwa Bi. Irene Mseluka ambaye amepata ujuzi wa kushona bidhaa mbalimbali za
ngozi na vitambaa akiwa gerezani katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji
Tanzania (TCT) Ukonga Jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri
Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akikagua Gwaride.
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na
Mfungwa Bi. Grace Chiduo ambaye amepata ujuzi wa kushona bidhaa mbalimbali
akiwa gerezani katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga
Jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri
Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza na Mfungwa Clemensia
Cosmas Mirembe (20) kwenye hafla hiyo. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa amesimama wakati wimbo wa
Taifa ukiimbwa kwenye hafla hiyo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye
picha na Wafungwa waliopata ujuzi wa ushonaji Gerezani Bi. Grace Chiduo (kulia)
na Bi. Irene Mseluka (kushoto) katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania
(TCT) Ukonga Jijini Dar es Salaam.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akisalimiana na viongozi
mbalimbali mara baada ya kuwasili katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji
Tanzania (TCT) Ukonga Jijini Dar es Salaam tarehe 09 Mei, 2026 kwa ajili ya
kuhitimisha Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu Kozi namba 28 na Uongozi Daraja la
Pili Kozi namba 48 kwa Mwaka 2025/2026. 
Viongozi wakishuhudia matukio mbalimbali katika
uwanja wa Gwaride wa Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga
Jijini Dar es Salaam.
Wahitimu wa Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu
Kozi namba 28 na Uongozi Daraja la Pili Kozi namba 48 ya mwaka 2025/2026 wakiwa
kwenye mkutano katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga
Jijini Dar es Salaam.
Wahitimu wa Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu
Kozi namba 28 na Uongozi Daraja la Pili Kozi namba 48 ya mwaka 2025/2026 wakiwa
kwenye mkutano katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania (TCT) Ukonga.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiwa kwenye picha na kikundi
cha burudani cha Wafungwa na Askari Magereza kwenye hafla ya kuhitimisha
Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu Kozi namba 28 na Uongozi Daraja la Pili Kozi
namba 48 ya mwaka 2025/2026 katika Chuo cha Taaluma ya Urekebishaji Tanzania
(TCT) Ukonga Jijini Dar es Salaam.
Wahitimu wa Mafunzo ya Uongozi Ngazi ya Juu Kozi
namba 28 na Uongozi Daraja la Pili Kozi namba 48 ya mwaka 2025/2026
wakivalishana vyeo katika hafla hiyo.





.jpeg)










0 Comments