.........................................
CHAMA Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimeingilia kati ukosekanaji wa mafuta nchini ambapo kimeishauri Serikali kutoa ruzuku ili kupunguza gharama za mafuta kama alivyofanya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan mwaka 2022 nchi ilipokuwa kwenye changamoto kama ilivyo hivi sasa.
Hayo yamebainishwa na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa
(NEC), Itikadi, Uenezi na Mafunzo,Kenani Kihongosi wakati akizungumza na waandishi wa habari Aprili 7, 2026, Jijini Dodoma.
“Tumeiagiza Serikali itoe ruzuku ili kupunguza gharama za mafuta kama ilivyofanywa mwaka 2022 wakati wa vita vya Urusi na Ukraine ambapo ilitoa Sh.Bilioni 100 hatua itakayo saidia kupunguza makali ya bei ya mafuta,” alisemaKihongosi.
Kihongosi aliongeza kuwa Serikali ipo katika mchakato wa kuanzisha
Mfuko Maalumu utakaosaidia kupunguza makali ya bei ya mafuta ambayo imepanda
kufuatia vita vinavyoendelea baina ya Israel, Marekani na Irani.
Alisema CCM na Serikali wamejipanga kuhakikisha mafuta yanapatikana wakati wote na kwa bei
nafuu ambapo alihimiza kubana matumizi ya safari za magari na kuelekeza katika
kipindi hiki magari ambayo yapo katika mfumo wa matumiziya gesi yatumie nishati
hiyo.
Alisema kuwa sababu ya kuongezeka kwa bei ya mafuta
imetokana na kufungwa kwa mkondo wa bahari
unaotumika kusafirisha mafuta kutoka Mashariki ya Kati kuja Afrika
Mashariki.
Kihongosi alieleza kuwa njia hiyo ya bahari hubeba takribani
asilimia 20 ya mafuta duniani hivyo kufungwa kwake kunaleta changamoto ya moja
kwa moja ikiwemo kupanda kwa bei ya mafuta.
Alisema kutokana na hali hiyo imesababisha bei ya mafuta
katika soko la dunia kupanda kwa kiasi kikubwa, kutoka dola za Marekani 700–800
hadi kufikia dola 1,700–1,800 ongezeko ambalo
limeathiri bei za ndani kwa
kupanda kwa zaidi ya shilingi 800 hadi 1,000 kwa lita.
Kihongosi aliongeza kuwa gharama ya “premium” imeongezeka
kutoka dola 80–110 hadi kufikia dola 270–300, hali iliyochangia ongezeko la
zaidi ya shilingi 200 kwa lita, na kufanya jumla ya ongezeko kufikia zaidi ya
shilingi 1,000.
Aidha, Kihongosi alisema kupanda kwa bei ya mafuta siyo kwa Tanzania pekee bali ni pamoja na baadhi ya nchi kama Zimbabwe, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Afrika Kusini ambapo bei imefikia takribani shilingi 5,000 kwa lita huku nchini Kenya, bei ikiwa kati ya shilingi 3,500 hadi 4,000 kwa lita.
Kihongosi alisema ukosekanaji wa mafuta haupo kwa nchi za Afrika pekee, bali pia katika nchi za Ulaya na Asia, akitolea mfano Uswisi akieleza kuwa bei ni kati ya shilingi 5,000 hadi 6,000 kwa lita, na Uingereza kati ya shilingi 5,500 hadi 6,500 kwa lita.
Waandishi wa habari wakichukua taarifa hiyo.
Taarifa hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990









0 Comments